TUWAFATILIE WANAFUNZI WANAOTAKIWA KURIPOTI KIDATO CHA KWANZA.
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari Kongwa DC
Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon Mayeka amewataka Waheshimiwa Madiwani, Watendandaji wa Vijiji na Kata pamoja na Walimu kwa ujumla kufuatilia kwa karibu wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2026 ili waweze kuripoti shule kuanza masomo na kupata haki yao ya msingi ya kupata elimu.
Mhe. Mayeka ameyasema hayo katika kikao cha Baraza la Madiwani cha robo ya pili inayoanza Oktoba hadi Desemba 2025 cha kujadili taarifa za kamati za kudumu za Halmashauri na taarifa za taasisi mbalimbali ambapo amesema kuwa suala la uandikishaji wanafunzi wa Awali, Msingi na Sekondari ni endelevu wanafunzi wote ambao bado hawajaripoti kidato cha kwanza wanafahamika hivyo wafatiliwe na kurudishwa shuleni.
Vilevile Mhe. Mayeka amemtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa kufuatilia kwa karibu suala la akaunti za Vijiji kama zinafanya kazi kama inavyotakiwa kwani kuna baadhi ya vijiji vina akaunti lakini hawazitumii ipasavyo suala linalopelekea matumizi ya fedha kutokuwa na utaratibu mzuri.
Akiongea katika kikao hicho mwakilishi kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Bw. amesema kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ameagiza Halmashauri kutoa elimu ya Bima ya Afya kwa wote kwa Wananchi ili waweze kuielewa, amesisitiza uandikishaji wa Wananchi katika daftari la wakazi na kusimamia miradi yote ya maendeleo ili iweze kukamilika ifikapo 30 Marchi Mwaka huu.
Nae Mbunge viti maalum Mkoa wa Dodoma Mhe. Jesca Mbogo amepongeza uongozi wa Wilaya ya Kongwa kwa jitihada kubwa unaofanya katika kuleta maendeleo kwa wananchi katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya maji kwani hali ya upatikananji wa maji katika Wilaya ya Kongwa kwa sasa haifanani na ya miaka ya nyuma.
Kwa upande wake meneja wa mamlaka ya Maji safi Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Kongwa Mhandisi Fransis Mallya amesema kuwa hali ya upatikanaji wa maji katika Wilaya ya Kongwa umefikia 64% licha ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali za wateja kutolipia ankara za maji kwa wakati.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.