MADIWANI KONGWA WAASWA KUDUMISHA UMOJA NA USHIRIKIANO
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari Kongwa DC
Madiwani wateule wa Kata 22 za Wilaya ya Kongwa pamoja na Madiwani wateule wa viti maalum wamekula kiapo cha uadilifu mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kongwa leo Desemba 05 2025, katika Mkutano wa kwanza wa Baraza la Madiwani Wilaya ya Kongwa uliohudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Wilaya, Mkoa pamoja na Wananchi.
Baada ya kula kiapo Waheshimiwa Madiwani wamepata fursa ya kupiga kura kumchagua Mwenyekiti pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa ambapo Mhe. White Zuberi Mwanzalila ameibuka kuwa mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti na Mhe. Richard Mwite ameibuka mshindi wanafasi ya Makamu Mwenyekiti.
Akiongea katika Mkutano huo mwakilishi wa Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Ndg. Peter Gujenji amewasisitiza Waheshimiwa Madiwani kuwa na umoja na ushirikiano kufanya kazi kwa bidi kwa mujibu wa sheria kanuni na taratibu za Halmashauri na kusisitiza Halmashauri kuhakikisha inawapatia Semina elekezi Madiwani hao ya kuwaelekeza namna ya uendeshaji wa shughuli za Kiserikali.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon Mayeka licha ya kuwapongeza Madiwani kwa nafasi waliyoipata ya kuaminiwa na Wananchi lakini pia amewataka kuvunja makundi yaliyojitengeneza wakati wa Uchaguzi na badala yake waungane kwa umoja wao ili wajikite katika kusimamia miradi ya maendeleo iliyopo katika Kata zao na kuhakikisha inakamilika kwa wakati na ubora unaotakiwa.
Akiwakilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Halmashauri katika kipindi ambacho Baraza la Madiwani lilikuwa limevunjwa, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa Dkt. Omary Nkullo amebainisha kuwa Halmashauri ilifanikiwa kutoa Milioni 632 kwa ajili ya kutekeleza shughuli za miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa jengo la upasuaji katika Kata ya Lenjulu.
Akiongea wakati wa kufunga mkutano huo wa Baraza la Madiwani, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa Mhe. White Zuberi amewashukuru Wananchi kwa kuwaamini na kuahidi kufanya kazi kwa bidii na umoja na kwa kushirikiana ili Wananchi wapate maendeleo.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.